ALIYEKUWA Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali (IGP), Omari Mahita, amemkana mtoto Juma Omari Mahita (8), anayedaiwa kuzaa na yaya wake, Rehema Shaabani.
Mahita, amemkana mtoto huyo kupitia utetezi wake aliowasilisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki kupitia kwa wakili wa kujitegemea, Charles Semigalawe.
Katika utetezi huo wa maandishi, Mahita ameieleza mahakama kwamba yeye si baba wa mtoto huyo.
Ameeleza kuwa madai ya mwanamke huyo kuwa Mahita, alikuwa Mkuu wa Polisi Mkoa (RPC) wa Kilimanjaro mwaka 1996, si ya kweli.
Utetezi huo umeeleza kwamba mlalamikaji alikuwa mtumishi wake wa ndani mwaka 1995, na hakuwa na mawasiliano naye baada ya kuacha kazi mwishoni mwa mwaka huo.
“Huyo Juma simtambui wala huyo mwanamke pia sina mawasiliano naye, tangu alipoacha kazi nyumbani kwangu mwaka 1995,” inasema sehemu ya utetezi huo.
Mahita, ameeleza kuwa mwaka 2003, akiwa IGP, mlalamikaji alifika nyumbani kwake Mtaa wa Bongoyo, Dar es Salaam na kufanya fujo akitaka Juma ahudumiwe.
Utetezi umeeleza kuwa, Mahita aliwaamuru askari wamfukuze mlalamikaji.
“Alipotoka kwangu alienda Ukonga nyumbani kwa dada yangu bila utambulisho wowote, alimwacha mtoto huyo… kwa huruma yangu niliamua kumpeleka mtoto huyo kwa Sheikh Yahaya Hussein ili ajifunze Kuran,” inasema sehemu ya utetezi huo.
Kesi hiyo namba 2/2006 ambayo ipo mbele ya Hakimu Mkazi, Pellagia Khaday, itasikilizwa leo.
Mahita anadaiwa kumtelekeza mtoto huyo. Mlalamikaji anaiomba mahakama imwamuru Mahita amlipe sh 100,000 kila mwezi kuanzia mwaka 1997, kama matunzo ya mtoto huyo hadi atakapohitimu shule.
Juma anasoma darasa la tatu katika Shule ya Msingi Muungano iliyopo Kinondoni, Dar es Salaam.
Maelezo ya mlalamikaji yanaonyesha kuwa uhusiano wa kimapenzi kati yao watu hao wawili ulianza Mei, 1996 hadi Oktoba, 1996.
Mlalamikaji anadai kwamba Mahita alimpa sh 40,000 na kushauriwa arudi nyumbani kwao Kondoa ili mkewe (ambaye sasa ni marehemu) asifahamu.
Mahita anadaiwa kufanya hivyo kwa ahadi kwamba angemlea mtoto atakeyezaliwa.
Katika kesi hiyo yenye mvuto kwa wakazi wa Dar es Salaam na vitongoji vyake, mlalamikaji anatetewa na Kituo cha Haki za Binadamu (LHRC).