Na Burhani Yakub,Tanga
KIASI cha Sh1 bilioni zinahitajika kwa ajili ya kukarabati jengo la kihistoria la Hospitali ya Bombo Cliff, lililojengwa wakati wa utawala wa Wajerumani kuanzia mwaka 1894 hadi 1903 lilipokamilika.
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Tanga ya Bombo, Magreth Mhando, alisema hayo juzi wakati akisoma taarifa kwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, aliyetembelea kukagua shughuli za upanuzi wa hospitali hiyo.
Alisema kutokana na umuhimu wa kutunza kumbukumbu za kihistoria ya nchini, kuna haja ya kulikarabatiwa jengo hilo ambalo lilipokamilika kujengwa lilikuwa na vitanda 21 vilivyokuwa kwa ajili ya kuwalaza wagonjwa wa kizungu tu.
“Ni jengo la Kihistoria linalochangia katika kumbukumbu ya utawala wa Wajerumani hapa nchini na lina usanifu wa kipekee unaoweza kuwa urithi kwa vizazi vijavyo,” alisema Mhando na kuongeza kuwa tathimini iliyofanyika inaonyesha ukarabati wa jengo hilo utagharimu Sh1 bilioni.
Mganga huyo aliiomba Serikali kupitia Wizara za Maliasili na Utalii, Twala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, kuona uwezekano wa kukarabati jengo hilo kwa faida ya sasa na vizazi vijavyo.
Mhnado alifahamisha kwamba, kwa sasa hospitali hiyo ina uwezo wa kuwa na vitanda 500, lakini vinavyotumika ni 380 tu kutokana na uchakavu na upungufu wa vifaa na watumishi, ambapo kuna wafanyakazi 340 kati ya 687 wanaohitajika.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Bartazal Ngoli, alisema kazi ya upanusi wa hospitali hiyo utakamilika Oktoba 2007 na itagharimu Sh780 milioni ambazo zimetolewa na Shirika la Fedha la Ujerumani (KFW).
Alisema katika mradi huo vinajengwa vyumba vya waganga wanaowahudumia wagonjwa wa nje, Kliniki za waganga mabingwa, kitengo cha kutakasia vifaa vya tiba, vyumba vitatu vya upasuaji, vyoo na sehemu za kubadili na kupumzikia wagonjwa.
Lowassa aliwashukuru wafadhili kwa msaada wao na kuwaomba kufikiria kama wataweza kusaidia ukarabati wa jengpo la kihistoria la Cliff.