KAMATI Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), inatarajiwa kukutana kesho chini ya Mwenyekiti, Rais Jakaya Kikwete.
Taarifa iliyotolewa jana na Katibu Mwenezi wa CCM, Aggrey Mwanri, inaeleza kuwa kikao hicho cha siku moja kimetanguliwa na kikao cha siku mbili cha Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa, ambacho ndicho kilichoandaa agenda ya Kamati Kuu.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa agenda zilizowasilishwa kwa Kamati Kuu na Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa ni pamoja na maandalizi ya uchaguzi mkuu wa CCM ambao utafanyika mwakani, kuanzia ngazi ya shina hadi taifa, uandaaji na uchaguzi katika mashina ya CCM nje ya nchi.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Kamati Kuu pia itapokea mapendekezo ya Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa kuhusu wanachama wa CCM wanaoomba kuteuliwa kugombea ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki.
Jumla ya wanachama wa CCM 49 kutoka nchi nzima wamejitokeza kuomba wateuliwe kugombea nafasi nane kati ya tisa zilizotengwa kwa Tanzania Bara katika Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Chama Cha Mapinduzi kina nafasi nane na upinzani ni moja, kutokana na uwiano wa idadi ya wabunge ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Miongoni mwa wabunge wanane watakaochaguliwa na wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuingia katika Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa tiketi ya CCM, watano watakuwa wanaume na watatu ni wanawake