SERIKALI imetakiwa kukiri kuwa ndani ya nchi hii kuna ubaguzi wa elimu baina ya Wakristo na Waislamu.
Wasomi mbalimbali, viongozi wa kisiasa na wanaharakati wamejenga hoja hiyo kwenye mjadala wa kujadili sera ya taifa ya elimu na kumkumbuka Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Washiriki hao, pamoja na mambo mengine, wameitaka serikali iingilie kati suala hilo, vinginevyo litailetea matatizo makubwa katika siku za usoni.
Mkufunzi wa Shirika la Elimu ya Sheria Tanzania (TANLET), George Kahangwa, ndiye aliyekuwa mtoa mada mkuu wa mjadala huo uliofunguliwa na Askofu mstaafu wa KKKT, Elinaza Sendoro, kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Manispaa ya Kinondoni, Dar es Salaam.
Hoja hiyo ilijengwa baada ya Mwenyekiti wa NCCR – Mageuzi, James Mbatia, kuibua hoja kuwa ndani ya taifa hili tayari kuna ubaguzi wa elimu kati ya Wakristo, hasa Wakatoliki na Waislamu. Washiriki hao walisema hoja hiyo inajadilika, kwa kuwa tangu nchi hii ipate uhuru haijawahi kujadiliwa kwa uwazi.
Mbatia alisema shule za Kikatoliki, kwa mujibu wa takwimu za Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), kila mwaka hufaulisha wanafunzi, huku shule nyingi za Kiislamu zikishika mkia, jambo ambalo alisema serikali isipoingilia kati na kulipatia ufumbuzi sasa, litaliletea madhara taifa siku za usoni, na kusisitiza kuwa hoja yake si ya ubaguzi wa kidini wala ya kuwafedhehesha Waislamu.
“Ili taifa liendelee ni lazima tuwe na moyo wa uzalendo na mwenye elimu amsaidie asiye na elimu, na tajiri amsaidie maskini…Serikali ikipuuzia haya, ni dhahiri huko tunakokwenda taifa litapata mpasuko kutokana na tatizo hili, kwa kuwa tayari kuna minong’ono kuwa Waislamu wanabaguliwa kwenye elimu ya juu na kufanya wasomi Waislamu kuwa wachache. Ninaomba nieleweke kuwa siwabezi Waislamu,” alisema Mbatia na kushangiliwa kwa makofi.
Naye Profesa Justinian Galabawa, wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alipendekeza ianzishwe sera itakayoruhusu wanafunzi kufundishwa maadili ya kitaifa, imani, uhuru na maadili yajengwe kwa mapana, yakilenga kujitegemea kuanzia ngazi ya familia na hadi shuleni, kwa sababu wanafunzi wengi hata waliopo vyuoni wana uwezo mdogo wa kufikiri na kusema, jambo ambalo ni hatari kwa taifa.
Sera ya elimu ya mwaka 1995 kwa mfano, haina matatizo makubwa, bali tatizo ni kwamba hizi zilizopo hazitekelezwi. Alisema duniani kote hakuna serikali inayotoa mikopo kwa wanafunzi waliofaulu kwa daraja la kwanza na la pili, bali hutoa mikopo kwa wahitaji, hivyo ni lazima wahusika wawe na fikra sahihi.
“Nyerere (Mwalimu Julius, Baba wa Taifa) alikuwa na fikra sahihi kwenye sera ya elimu, ndiyo maana hatutofautiani naye, hivyo Watanzania lazima wafundishwe imani, motisha zao zipo wapi na wajengewe uwezo kutoa maoni yao na kufikiri. Ila ndiyo hivyo, siku hizi ukionekana wewe ni mchambuzi wa mambo zaidi unafukuzwa kazi au shule,” alisema Profesa Galabawa.
Naye kiongozi na mwanasiasa wa siku nyingi, Dk. Hassy Kitine, aliishauri serikali kupitia wataalamu wake, ifanye utaratibu wa kuuliza shule za Kikatoliki zinatumia mbinu zipi hadi zinafanikiwa na wakishapata mbinu hizo zichukuliwe na kupelekwa kwenye shule za Kiislamu ili nazo zizitumie na kufanikiwa ili hatimaye taifa liwe na wasomi wa kutosha kutoka dini zote mbili.
Mwanasheria na Wakili wa Kujitegemea, Said Hamad El – Maamry, aliunga mkono hoja ya Mbatia, na kusema ukweli lazima uzungumzwe ili ufumbuzi upatikane na shule za Waislamu zifanye vizuri kielimu.
“Tusilete tabaka la udini, bali tulete tabaka la ukweli kwa ajili ya masilahi ya taifa hili. Hoja ya Mbatia ni nzito na imejaa ukweli mtupu, hivyo serikali haina budi kuchukua juhudi za kusaidia Waislamu ambao ukweli ni kwamba shule zao hazifanyi vizuri kwenye mitihani,” alisema El – Maamry.
Naye mchumi na mwanasiasa wa siku nyingi, Idd Simba, alisema hii ni mara ya kwanza kwa nchi hii tangu ipate uhuru kuwa na mjadala kama huo, na akawataka washiriki na Watanzania kwa ujumla wawe wazi katika kulipatia ufumbuzi suala hili la sera ya elimu hapa nchini.
Simba alisema pande hizi mbili zinaongoza waumini wao kwa utaratibu unaotofautiana, kwa kuwa Wakatoliki tangu enzi za ukoloni walikuwa na mtandao mzuri ambao umewawezesha hata shule zao kufaulisha vyema, tofauti na shule za Kiislamu, kwani tangu kipindi hicho hadi sasa hakuna mtandao waliojiwekea.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha National League for Democracy (NLD), Emmanuel Makaidi, alisema kinachowafanya Watanzania waendelee kumkumbuka Mwalimu Nyerere ni uongozi wa nchi hii kupwaya. Alisema robo tatu ya viongozi wa serikali ya sasa ni wanajeshi, nchi inaongozwa kijeshi na kazi ya viongozi hao ni kutoa amri, si kufuata sera wala sheria, ndiyo maana hata utaratibu wa kutoa mikopo kwa wanafunzi umekwenda kinyume cha Sheria ya Bodi ya Mikopo na umewagawa Watanzania.
Mwenyekiti wa Tanzania Labour Party (TLP), Augustine Mrema, ambaye kabla ya kuanza kuchangia hoja alishangiliwa kwa makofi na vigelele na washiriki, alisema alikuwa anafahamu kuwa mpasuko upo Zanzibar peke yake, ila kupitia mjadala huo, amefahamu kuwa hata Tanzania Bara kuna mpasuko wa ubaguzi wa elimu kwa pande hizo mbili - Waislamu na Wakristo.
“Kwa kweli huu mjadala mlioanzisha ni mzito sana, na unahitaji kuvaliwa njuga, na siku nyingine mumualike Rais (Jakaya) Kikwete na Lowassa (Edward, Waziri Mkuu), wakae kwenye viti kule nyuma kama washiriki wengine, wasikilize wananchi wao wenye uchungu wa nchi hii wakichangia mjadala huu …kwa kuwa hawa viongozi kazi yao kubwa ni kuzurura na kujifanya wanahutubia wananchi,” alidai Mrema huku washiriki wakivunjika mbavu kwa kicheko.
Naye Sheikh Khalifa Khamis, alisema hoja hiyo ya ubaguzi wa elimu ni ya msingi, na kwamba serikali iliipuza tangu miaka ya nyuma.
Mkurugenzi wa TANLET, Dk. Sengondo Mvungi, aliahirisha mdahalo huo hadi Novemba 4 mwaka huu, akasema shirika lake lipo tayari kupokea maoni tofauti kutoka kwa Watanzania wenye nia njema na Tanzania ili kuijenga