Na Mwandishi Wetu
SERIKALI ya Jamhuri ya Korea Kusini imesema italitafakari na kulipa uzito wa pekee ombi la Rais Jakaya Kikwete la msaada wa ujenzi wa daraja katika Mto Malagarasi, mkoani Kigoma.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Ikulu mjini Dar es Salaam ilisema kuwa Rais Kikwete alitoa ombi hilo jana alipokutana na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Jamhuri ya Watu wa Korea Kusini, Ban-Ki-Moon.
Moon alisema kuwa serikali yake italijenga daraja hilo kwa mkopo nafuu sana pale mambo yote yatakapokubalika. Mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu yaligusa zaidi uhusiano kati ya nchi hizo.
Alisema serikali yake itaendelea kusaidia Tanzania katika uendeshaji wa vyuo vya ufundi stadi sambamba na utoaji wa vifaa vya teknolojia ya mawasiliano.
Moon alisema Korea Kusini inaridhishwa na kasi aliyoanza nayo Rais Kikwete na kuongeza kuwa itatoa ushirikiano ili kuhakikisha kuwa anatekeleza kile alichoahidi kwa Watanzania.
Awali, Rais Kikwete aliiomba serikali ya Korea Kusini kusaidia ujenzi wa daraja la Mto Malagarasi ambalo alisema ni muhimu kwa maendeleo ya mkoa wa Kigoma na Tanzania kwa jumla.
Rais Kikwete alisema kuwa kukamilika kwa daraja hilo kutafungua milango ya mawasiliano na biashara kati ya Tanzania na nchi jirani.
Pia, alitumia fursa hiyo kuishukuru serikali ya Korea Kusini kwa kusudio lake la kuendesha na kusaidia elimu ya ufundi stadi nchini.
Alisema kuwa vyuo vya elimu ya ufundi stadi ni muhimu katika kuwapa fursa wanafunzi ambao hawakuweza kuendelea na elimu ya juu na kwamba elimu ya ufundi ni muhimu kwa maendeleo ya nchi.