MSAFARA wa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, umekwama wilayani Kilindi ulipokuwa ukienda kwenye mkutano wa hadhara uliokuwa ufanyike katika Tarafa ya Kimbe.
Msafara huo ulilazimika kuishia katika Kijiji cha Legero, maili 25 kuelekea katika tarafa hiyo.
Kukwama huko kumetokana na ubovu wa barabara kutoka Morogoro hadi Handeni yenye urefu wa kilometa 70.
Mkuu wa Wilaya ya Kilindi, Sarah Dumba, alilazamika kwenda kuitwa kutoka Kimbe ambako alikuwa amewakusanya wananchi kwa ajili ya kusubiri mkutano huo.
Miongoni mwa viongozi waliokuwamo kwenye msafara huo ambao walishuhudia adha hiyo ni Naibu Waziri wa Miundombinu, Dk. Milton Mahanga.
Akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Legero, Waziri Mkuu alikemea tabia ya baadhi ya wakzi wa Handeni kuuza mazao yao kwa bei rahisi, kisha baadaye kuuziwa mazao hayo kwa bei ya juu.
Alitoa mfano kuwa wanauza mahindi kwa sh 12,000 kwa gunia, baada ya msimu wanauziwa mahindi hayo kwa sh 35,000 kutokana na kutokuwa na akiba ya chakula. Aliwahimiza kuhifadhi chakula.
Hata hivyo, mkutano huo ulifanyika bila kuwapo kwa mkuu wa wilaya wa eneo hilo, kwani alikuwa Kimbe, ambako awali mkutano huo ulipangwa kufanyika.