MWENYEKITI wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustino Mrema, amesema hatamzika mwanamke aliyezaa naye, Angelina Mosha.
Akizungumza na waandishi wa habari, katika Makao Makuu ya TLP, yaliyopo Magomeni Dar es Salaam, Mrema alisema kuwa hatamzika mwanamke huyo kwa kuwa alishatubu kwa mkewe na kanisani.
“Siwezi nikapanda gari hadi Moshi kwa ajili ya hawara ambaye alikuwa hajithamini. Angekuwa mke wangu angetumiwa na makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwa ajili ya kunirubuni katika kipindi cha kampeni cha mwaka 1995?” alisema Mrema.
Alisema anawashangaa wana CCM, kuwa si watu wenye utu, kwa kuwa wakati wa kampeni alikuwa ni mwanamke mzuri sana wa kumtumia katika kumchafulia jina lake, lakini sasa wameshindwa kumzika.
Mrema alilitupia lawama Jeshi la Polisi nchini kwa kushindwa kufanya kazi yake inavyotakiwa, na matokeo yake kutoa taarifa za juu juu kuhusu kifo hicho ambazo hazina ukweli.
“Polisi walitakiwa kufanya upelelezi na kubaini katika nyumba ya wageni alipokwenda kupanga alikuwa ameenda na nani na ni nani ambaye alikuwa anamlipia fedha ya pango,” alisema Mrema.
Pia alishangazwa na kitendo cha mwili wa Angelina kukaa hospitalini muda mrefu, kwani kwa kawaida maiti huhifadhiwa hospitali kwa muda wa wiki moja na iwapo ndugu hawajatokea huzikwa na Jiji.
Wakati huohuo, habari za kuaminika kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) zinaeleza kuwa, mwili wa Angelina umechukuliwa jana hospitalini hapo na ndugu wa marehemu kwa ajili ya mazishi mjini Moshi.
Angelina alifariki dunia Septemba 12, mwaka huu katika nyumba ya wageni ya A.M iliyopo Kawe Kisalasala, Dar es Salaam. Maiti hiyo ilihifadhiwa hospitalini hapo tangu wakati huo hadi jana ilipochukuliwa na ndugu zake