MBUNGE wa Viti Maalumu, Amina Chifupa, jana alinunua tiketi za Bahati Nasibu ya Mwalimu Julius Nyerere 5,200, zenye thamani ya sh milioni 2.6 na kuzikabidhi kwa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM).
Chifupa alikabidhi tiketi hizo ambazo zitagawanywa katika mikoa yote nchini, katika ofisi za UVCCM kisha zitagawanywa katika kila wilaya za mkoa.
Akizungumza jana wakati akikabidhi tiketi hizo katika hafla iliyofanyika katika ofisi za Umoja wa Vijana Dar es Salaam, Chifupa alisema nia yake ni kumuenzi hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, ambaye alifariki dunia miaka saba iliyopita.
Alisema endapo tiketi hizo zitashinda, zawadi yoyote itakayopatikana, itakuwa mali ya mkoa ambao umeshinda, na hiyo ndiyo zawadi yake ya kumbukumbu ya maadhimisho ya siku hiyo.
Droo ya shindano hilo inatarajiwa kuchezeshwa Oktoka 14, mwaka huu katika Uwanja wa Nyamagana, Mwanza.
Droo kubwa ya bahati nasibu hiyo itachezeshwa siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa Nyerere Aprili 13 mwakani. Washiriki watashindana kupata gari kubwa aina ya Scania. Tiketi hizo alikabidhiwa Katibu wa Idara ya Mipango ya UVCCM Taifa, Ally Issa.