WANANCHI wa Wilaya ya Nkinga, wamemzomea waziwazi Mbunge wao, Mbaruk Mwandoro (CCM), mbele ya Waziri Mkuu, Edward Lowassa, wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Kata ya Malamba jana.
Wananchi hao walipaza sauti zao mbele ya Waziri Mkuu wakidai kuwa mbunge huyo, amewasahau na hana msaada kwao, hasa aliposhindwa kusimamia makao makuu ya wilaya mpya ya Nkinga kujengwa kwenye kata yao.
Walisema makao makuu hayo yanayojengwa Kata ya Kasera, maamuzi yamefanywa kwa upendeleo, na kwamba eneo hilo halina miundombinu wala huduma zozote za barabara.
Walidai kuwa mbunge huyo hajawahi kufika kwao tangu achaguliwe, licha ya kwamba walimpa kura nyingi, na hivyo alitakiwa afike ili wajadiliane kuhusu mambo mbalimbali ya maendeleo, ikiwa ni pamoja na hilo la makao makuu ya wilaya.
“Hafai huyo, hana lolote, ameshindwa kututetea ...haonekani kwenye jimbo lake,” walisikika wananchi wakisema kwenye mkutano huo.
Walisema walimpigia kura mbunge huyo kwa kukilinda chama, lakini hawana mapenzi naye.
Waziri Mkuu kwa upande wake aliwauliza wananchi hao wana kisa gani na mbunge wao kiasi cha kumzomea hivyo hadharani.
Aliwaambia kwa kuwa tayari wamekwishamchagua kama mbunge wao, hivyo hawana jinsi tena, na kwamba wanachotakiwa ni kushirikiana naye ili awaletee maendeleo.
“Msiutumie mkutano wangu kumzomea mbunge wenu, tafuteni muda wenu kuongea naye, na si mkutano wangu,” Waziri Mkuu aliwasihi.
Hata hivyo, alimgeukia mbunge huyo na kumtaka afanye mikutano mara kwa mara na wananchi hao, ili kusikiliza matatizo yao na kutatua kero zao.
Aliwaambia wafute mawazo ya kuhakikisha makao makuu ya wilaya yanajengwa kwao, kwa kuwa serikali imekwisha kutoa sh milioni 500 kujenga makao hayo.