MBUNGE wa Muheza, Hebert Mtangi, ameahidi kutoa mifuko 50 ya saruji kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa shule ya sekondari ambayo inatarajiwa kujengwa katika Kijiji cha Mwembeni, Kata ya Magoroto wilayani hapa.
Mtangi alitoa ahadi hiyo juzi alipofanya ziara yake ya siku moja ya kuwashukuru wananchi wa kijiji hicho kwa kumchagua pamoja na kuhamasisha maendeleo katika jimbo hili.
Alisema ameamua kufanya hivyo kwa sababu kata hiyo haina shule ya sekondari, kitu ambacho kinafanya wanafunzi ambao wanamaliza elimu ya msingi kupata tabu ya kwenda kusoma shule za mbali.
Mbunge huyo aliwataka wananchi wa kata hiyo kujitolea nguvu zao katika ujenzi wa sekondari hiyo ili umalizike mara moja, na wanafunzi watakaofaulu waweze kujiunga katika sekondari hiyo.
Wananchi hao walimhakikishia mbunge huyo kuwa wapo tayari kuchangia kufanikisha ujenzi huo, lakini wamechoka, kwa kuwa awali uongozi wa kijiji hicho uliwachangisha fedha kwa ajili ya ujenzi wa sekondari hiyo, lakini fedha hizo zilitafunwa.
Kwa upande wake, mbunge huyo aliwashauri wananchi hao kutokata tamaa na kuendelea kuchanga kwa ajili ya ujenzi wa sekondari hiyo, na kwamba kiongozi yeyote atakayekula fedha za wananchi atachukuliwa hatua kali za kisheria