MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro, amesema ameunda tume ya kuchunguza ufisadi unaofanywa na wafanyabiashara wakubwa ambao wanawatumia wafanyabiashara wadogo wadogo (wamachinga) kwa lengo la kukwepa kodi.
Alisema jana kuwa, uchunguzi uliofanywa na baadhi ya watendaji wa serikalini, umebaini kuwa wamachinga waliokuwa wamezagaa katika mitaa mbalimbali ya jiji, ukiwamo Mtaa wa Kongo, walikuwa wakitumiwa na baadhi ya wafanyabiashara wenye mitaji mikubwa kwa lengo la kukwepa kodi.
Kandoro alisema endapo mfanyabiashara yeyote atabainika kufanya kitendo hicho, atachukuliwa sheria kali kwa kuwa atakuwa ameiibia serikali kwa kukwepa kodi.
“Wamachinga wengi ambao walikuwa wanafanya fujo, na ambao walikuwa hawataki kutulia katika maeneo, ni wale ambao walikuwa wanatoa bidhaa katika maduka ya wakubwa,” alisema Kandoro.
Aliwasihi wafanyabiashara hao kukaa katika maeneo yao waliyopangiwa, ili waweze kusaidiwa hata kwa kupatiwa mikopo wakiwa katika vikundi.