MKURUGENZI wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Martina Kabisama, ametaka kulipwa fidia ya sh milioni 100 kwa madai ya kukashifiwa kwamba alitumia fedha za jumuiya hiyo kumjengea nyumba na kumnunulia gari hawara yake.
Mdai huyo, anayetetewa na Wakili wa kujitegemea Samson Mbamba, amefungua kesi namba 269/2006 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, akitaka fidia hiyo kutoka kwa Pilly Marwa, anayetetewa na Kampuni ya Uwakili ya Sekaboy.
Hati ya madai iliyowasilishwa mahakamani na Kabisama, ambaye ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Maendeleo ya Wanawake, Watoto na Jinsia katika CCT, imeeleza kwamba Julai 15 mwaka huu, mlalamikiwa (Pilly), alimwandikia barua mlalamikaji akimshutumu kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mumewe, Idrissa Mtulia Shamte.
Hati ya madai inaeleza kwamba, nakala ya barua hiyo ya kashfa ilisambazwa kwa watu binafsi, akiwamo mume wa mlalamikaji, William Kabisama, Mwenyekiti, Katibu Mkuu wa CCT na mashirika binafsi, ikieleza namna alivyotimiza mipango ya kumjengea nyumba mkoani Morogoro na kumnunulia gari Shamte, kwa fedha za CCT.
Mlalamikaji ametoa maelezo kwamba, barua hiyo haina ukweli, imeharibu uhusiano wake kwa mume na familia ya mumewe, kwani anaonekana si mwaminifu kwenye ndoa yake na ni mfujaji wa fedha za waumini wa CCT.
Aidha, maelezo hayo yanaendelea kusema kwamba, mlalamikaji hamfahamu mlalamikiwa, pia kashfa hizo zimepoteza uaminifu wa mlalamikaji kutoka kwa wafanyakazi wenzake wa Dodoma na jumuiya nzima ya Wakristo.
Hati hiyo ya madai pia imeeleza juhudi za mlalamikaji kutaka kuombwa radhi bila mafanikio, ambapo mlalamikiwa amekuwa akisisitiza madai hayo na kuzidi kuchafua jina la mlalamikaji.