SERIKALI imepanga kujenga bustani ya kumbukumbu ya kumuenzi Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, itakayogharimu jumla ya dola mil 4 (zaidi ya sh bilioni 5).
Bustani hiyo inatarajia kujengwa mbele ya kiwanja cha wazi kilicho mbele ya nyumba yake, kiwanja ambacho kilikuwa kimevamiwa na mfanyabiashara aliyeweka makontena na kufyatua matofali.
Habari kutoka Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNH), zinasema kwamba kibanda cha kioo kilichotumika wakati wa kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa Mwalimu baada ya kifo chake kilichotokea Hospitali ya St. Thomas, Uingereza, kitawekwa katika bustani hiyo.
Mradi huo umetambulishwa kama Ustawishaji wa Bustani ya Kumbukumbu ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius K. Nyerere, au Mwalimu Nyerere Memorial Park, na umelenga kwa ajili ya Watanzania wote na wapenda amani kote ulimwenguni.
Katika bustani hiyo kutakuwa na maktaba ambayo itawekwa vitabu vya Mwalimu Nyerere, magazeti na vitu vyake vya kihistoria, pia kutakuwa na mgahawa kwa ajili ya wageni.
Bustani hiyo itakuwa na vikundi vya burudani asilia vitakavyokuwa vikitoa burudani ya ngoma za asili na burudani hiyo itakuwa katika mahadhi ya Kiafrika, Kiasia na Ulaya.
Katika bustani hiyo kutakuwa na kiwanja cha michezo ya mpira wa miguu kwa watoto na watu wazima, na pia kutakuwa na mchezo wa bao katika kibanda cha asili cha msonge. Mwalimu alikuwa mchezaji na mpenzi mkubwa wa mchezo wa bao.
Mradi huo utatekelezwa katika hatua mbili. Hatua ya kwanza itakayogharimu dola 272,000 (sh zaidi ya milioni 354) imepangwa kuanza Septemba 2006 hadi Machi 2007. Hatua ya pili ya mradi huo imepangwa kuanza Januari 2007 na itagharimu dola 250,000 (sh zaidi mil 325).
Wahandisi wanaohusika na mpango huo ni TMK Contractors Ltd iliyopo Manispaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam. Wahamasishaji wa mradi huo ni Taasisi ya Mwalimu Nyerere na unasimamiwa na serikali yenyewe.
Mwalimu Nyerere alifariki mwaka 1999 akiwa na umri wa miaka 77, na kila mwaka Oktoba 14 huwa Siku ya Baba wa Taifa, ambayo huadhimishwa kitaifa kwa mapumziko na kufanya shughuli za kumkumbuka.