Baada ya kusota kwa muda mrefu bila kuwa na ofisi, hatimaye ushirika wa viwanda vidogo Jijini Dar es salaam, DASICO hivi karibuni wanatarajia kujenga jengo la ghorofa nne litakalogharimu kiasi cha sh. bilioni 1 na milioni 425, ukiwa ni mpango wa maendeleo wa ushirika huo.
Akizungumza katika mkutano mkuu wa DASICO, Mwenyekiti wake Bw. Mfaume Yusufu, amesema tayari wameshaandaa michoro ya ramani ya jengo hilo na na hivi sasa wanasaka wawekezaji baada ya kupata ridhaa ya wanachama.
”Huo ni mpango mmojawapo wa maendeleo kati ya kadhaa tuliyojipangia. Tumeamua kuuleta kwenu kisha tutafute wawekezaji baada ya kupata ridhaa yenu wanachama kabla ya kuendelea na hatua nyingine,” amesema Bw. Yusuf.
Bw. Mfaume amesema ushirika huo una mipango mingi ya maendeleo na wataendelea kupiga hatua moja baada ya nyingine ili ushirika wao uweze kufanikiwa.
Akizungumzia upande wa ushirika wa kuweka na kukopa SACCOS, Mwenyekiti huyo amesema wamefanikiwa kuanzisha ushirika huo wa kuweka na kukopa na hivi sasa tayari wamepata usajili wa kudumu.
”Hata uanzishwaji wa Saccos ni mpango wetu mwingine wa kimaendeleo.
Tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa huku mambo mengine tukitarajia kuyakamilisha baadaye, kwanini tushindwe?” akasema Mwenyekiti huyo