Mfululizo wa vifo vya makumi ya watu kupitia vyombo vyetu mbalimbali vya usafiri nchini umeendelea kushika kasi na kuacha wafiwa wakitaharuki.
”My God! Ni mkosi gani huu?” Wengine wamediriki kujiuliza kwa mshangao pasi na kupata jibu la maana.
Ajali mbaya iliyotokea mkoani Singida na kukatiza maisha ya watu wanane na kujeruhi wengine kadhaa kufuatia lori la Jeshi la Magereza kupinduka ni mfululizo wa vilio hivi vya kuhuzunisha.
Awali, mwishoni mwa wiki iliyopita iliripotiwa ajali mbaya ya basi la Champion lililokuwa likielekea Dodoma toka Dar na kuua watu 17 huku zaidi ya 40 wakiwa taabani kwa majeruhi.
Na wiki hii juzi tena, kukatokea ajali mbaya ya kiberenge kilichokatiza uhai wa watumishi 7 wa Shirika la Reli nchini waliokuwa kwenye kiberenge wakati wa kazi zao ambacho chenyewe kiligongana uso kwa uso na treni.
Kuhusiana na ajali hii ’latest’ iliyotokea Singida, Polisi mkoani humo imeyataja majina ya watu wanane waliofariki hadi sasa.
Waliokufa katika ajali hiyo ni pamoja na Askari Magereza ? Koplo Athuman Hassan wa Gereza la Komboi, Koplo Michaek Mgaza na WDR Hassan Sadiki wa Gereza la Ushora.
Wengine waliofariki ni Mchungaji wa Kanisa la Angilikana la Ubungo Jijini Dar es Salaam Bw. Baraka Klasi.
Wakatajwa wengine kuwa ni mfungwa Samwel Selemani, mkazi wa Singida Mjini Bw. Moshi Amiri,14, Bw. Bakari Selemani ,18 ambaye ni mkazi wa kijiji cha Ushora na Bw. Athumani Juma, mkazi wa kijiji cha Nguvumali, kata ya Ndago wilayani Iramba.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani Singida, Bi. Celina Kaluba ajali hiyo ilitokea saa 2.30 usiku katika kijiji cha usure kata ya Ndago, wilayani Iramba kwa kuhusisha lori hilo la Magereza, Isuzu lenye namba za usajili STK 1669.
Majeruhi waliotajwa katika katika ajali hiyo ni Mkuu wa Gereza la Ushora Bw. Mohamed Matimula na askari wa Magereza wa mjini Singida Bw. Seleman Ibrahim.
Wengine ni wafungwa Paulo Joh,23, na Hamis Salim pamoja na mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Al Hazary inayomilikiwa na Msikiti wa Kati Mjini Singida, Gasper Joackim,17.
Hata hivyo, akasema majeruhi wengine katika lori hilo lililokuwa likiendeshwa na Koplo Salum wameshatibiwa na kuruhusiwa kurejea makwao.
Kamanda Celina akasema watu hao walikufa kutokana na kukandamizwa na magunia ya unga yaliyokuwa yakipelekwa kwenye gereza la Ushora na wengine kukaliwa na lori hilo lililopasuka tairi la nyuma kabla ya kupinduka.