CHAMA cha Wananchi (CUF), kimemshutumu Rais Jakaya Kikwete kwa ukaribu wake na Rais George W. Bush wa Marekani kwa madai kuwa unampotezea uwezo wa kutetea wanyonge.
Akizungumza na waandishi wa habari, Makao Makuu ya CUF Buguruni, Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema ukaribu wa Rais Kikwete kwa Bush unatia shaka kwa taifa kwa vile unapoteza falsafa iliyoasisiwa na Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere juu ya kuwa msemaji wa wanyonge katika duru za kimataifa na kusisitiza manufaa ya Tanzania.
“Ukaribu huu wa Rais Kikwete kwa Rais Bush unatia shaka kwa kumpotezea uwezo wa kutetea wanyonge kama Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alivyoasisi sera iliyotujengea heshima kubwa katika mataifa makubwa ulimwenguni,” alisema Profesa Lipumba.
Alisema moja ya haki ni kama ile ya kuwatetea Wapalestina kuchagua viongozi wanaowataka, kulaani mashambulizi ya kinyama ya Israel dhidi ya Lebanon na kuunga mkono haki za Iran kufanya utafiti wa matumizi ya amani ya nguvu za nyuklia.
Alisema Rais Kikwete hawezi kueleza hadharani kuwa Marekani inavunja sheria za kimataifa kwa kuivamia Iraq bila idhini ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wakati ilikuwa haina silaha za maangamizi.
“Uamuzi wa Rais Kikwete unaweza kuwa ni mkakati wa kuanza kuachana na sera za Mwalimu Nyerere kuwa msemaji wa wanyonge katika duru za kimataifa na kusisitiza manufaa ya Tanzania nje,” alisema Profesa Lipumba.
Alisema Rais Bush hayuko mstari wa mbele katika kulisaidia Bara la Afrika ambapo ahadi zake za Monterey za kuongeza misaada hazijatekelezwa.
“Pamoja na kuweka saini makubaliano ya kimataifa ya nchi tajiri kuongeza misaada yake kwa asilimia 0.7 ya pato la taifa kama msaada kwa nchi maskini, Marekani haijafikia lengo hili na inatoa asilimia 0.2 ya pato la taifa,” alisema Profesa Lipumba.
Wakati huo huo, CUF imemtaka Rais Kikwete, aitishe mkutano wa kitaifa wa viongozi wa vyama vya siasa na wataalamu wa uchumi ili kujadili hali ya uchumi wa taifa.
Profesa Lipumba alisema mkutano huo utatoa fursa kwa viongozi na wataalamu wa masuala ya uchumi kuweka mikakati madhubuti ya kupambana na hali mbaya ya umaskini.
“Tunatoa mwito kwa Rais Kikwete kuitisha mkutano wa kitaifa wa viongozi wa vyama vya siasa, taasisi za kijamii na wasomi wa hapa nchini ili kubadilishana mawazo juu ya jinsi gani taifa letu linaweza kukabiliana na matatizo makubwa ya kiuchumi na kijamii yanayolikabili na kuendelea kuathiri maisha ya Watanzania, hasa wale walio masikini kwa asilimia 50,” alisema Lipumba.
Mtaalamu huyo wa uchumi aliyepata kuwa mshauri wa uchumi wa rais nchini Tanzania na Uganda, alisema sambamba na hatua hiyo ya kuhitaji mkutano huo wa kitaifa, Rais Kikwete anatakiwa kuwaita wamiliki wa benki zote, ili azungumze nao juu ya utoaji mikopo kwa wafanyabiashara wadogo.
“Mabenki yetu yameshindwa kuwa wazi juu ya utoaji wa mikopo kwa wafanyabiashara wetu wadogo, hali ambayo imeleta umaskini mkubwa bila sababu yoyote,” alisema Lipumba.
Aliongeza kuwa, matatizo hayo yamechangiwa na urasimu na gharama kubwa ya kuanzishwa na kusajili kampuni, kupata leseni. Alisema kuwa, taratibu mbovu za kupata haki za kumiliki mali ni chanzo kikubwa cha kushuka kwa uchumi wa taifa