MAELFU ya watu wa kada mbalimbali, jana walijitokeza kwa wingi katika shughuli za mazishi ya vijana wawili wa Kitanzania, mtu na mchumba wake, waliouawa kikatili nchini Marekani siku 15 zilizopita.
Katika viwanja vya Leaders, Kinondoni, Dar es Salaam, zilikoanza kufanyika shughuli za kuwaaga marehemu hao wawili, Walter Mazula (28) na Vonetha Nkya (28), hali ilikuwa ni ya simanzi na mara kadhaa vilio vya kwikwi vilisikika.
Miongoni mwa watu waliohudhuria maombolezo na hatimaye mazishi hayo ni Waziri Mkuu, Edward Lowassa na mkewe Regina; mke wa Rais, Salma Kikwete; mke wa Rais mstaafu, Anna Mkapa na Rais wa Bunge la Afrika, Getrude Mongella.
Wengine waliohudhuria mazishi hayo yaliyofanyika makaburi ya Kinondoni, Dar es Salaam, ni Mwenyekiti wa Taifa wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba; Mwenyekiti wa Taifa wa NCCR Mageuzi, James Mbatia, mawaziri wakuu wastaafu, Joseph Warioba na Salim Ahmed Salim, kwa kuwataja wachache.
Hali ilikuwa ni ya majonzi mazito wakati baba wa marehemu Walter, Kapteni George Mazula, alipopewa nafasi ya kuzungumza kuhusu tukio la kuuawa kwa mwanawe na mchumba wake lililotokea Septemba 22 huko Detroit, Michigan walikokuwa wamekwenda kwa masomo.
Alipohitimisha hotuba yake iliyobeba ujumbe mzito kwa maneno yasemayo; ‘Walter alikuwa ni rafiki yangu’, watu waliohudhuria msiba huo, walisikika wakitoa sauti za vilio na kusikitika.
Kapteni Mazula, mmoja wa marubani wa muda mrefu hapa nchini, alisema siku ya tukio, wachumba hao wawili waliokuwa wakiishi Detroit waliamka asubuhi kwa ajili ya kwenda kazini.
Alisema kabla ya Mazula kumpeleka mchumba wake Vonetha kazini, kwanza alimpitisha saluni kwa ajili ya kutengeneza nywele.
Alisema rafiki wa Vonetha ambaye walikuwa wakifanya kazi pamoja, aliingiwa na wasiwasi wa kutokumuona rafiki yake kazini hadi saa 9:00 mchana, hivyo aliamua kumpigia simu ili kufahamu kama alikuwa na tatizo.
Alisema hata hivyo alianza kuingiwa na wasiwasi baada ya kushindwa kumpata kupitia katika simu yake, pamoja na ile ya mchumba wake.
Baada ya kuona hivyo aliamua kuwasiliana na ndugu wa marehemu hao, ambaye alikuwa akiishi nao, ili kupata taarifa zaidi za wachumba hao.
“Ndugu huyo hakuwa na jibu zaidi ya kusema kuwa aliwaacha nyumbani. Kutokana na hali hiyo, aliamua kutoa taarifa katika kituo cha polisi, na kesho yake, yaani Septemba 23, walipata taarifa kuwa miili ya wawili hao, ilionekana katika maeneo tofauti wakiwa wamekufa,” alisema Mazula.
Alisema mwili wa marehemu Vonetha, ulikutwa ndani ya gari ambalo lilikuwa likiwaka moto wakati mwili wa marehemu Walter ulikutwa umetupwa sehemu nyingine, ukiwa pembezoni mwa barabara.
Akitoa wasifu wa marehemu hao, ndugu wa marehemu Walter, George Mazula alisema wachumba hao walichumbiana mwaka jana na walikuwa na mpango wa kufunga ndoa mwishoni mwa mwaka huu.
“Walikuwa wachangamfu na walikuwa wakishirikiana na watu wote walipokuwa hapa nchini na hata huko Marekani bila kujali utaifa wao. Walikuwa na mipango mingi mizuri ya maisha,” alisema.
Wachumba hao, walizaliwa Machi mwaka 1979, lakini walitofautiana kidogo kwa tarehe ya kuzaliwa kwani, Vonetha alizaliwa machi 12 na Walter machi 5.
Taarifa kutoka Marekani zinaonyesha kwamba, Watanzania wanaoishi Marekani, walipatwa na mshtuko mkubwa kutokana na mazingira na vifo vya wenzao hao ambao salamu zilizosambaa katika mtandao wa intaneti zinaonyesha kwamba walikuwa marafiki wa kila mtu.
Wakiwa katika hali ya majonzi, waliamua kufungua akaunti maalumu ya kukusanya fedha kwa ajili ya kuweza kumudu gharama zote kutunza na kusafirisha miili ya marehemu hao ambazo zilikadiriwa kufikia dola za Marekani 20,000 (sawa na sh milioni 25.6).
Akaunti hiyo iliyofunguliwa chini ya jina la Walter Mazula & Vonetha Nkya Trust Fund TCF National Bank Account Number: 6869101756 Route Number: 291070001 ndiyo ambayo ilionekana ingeweza kwa kiwango kikubwa kufanikisha shughuli nzima ya kusafirisha miili hiyo hadi Dar es Salaam.
Akizungumzia tukio hilo siku chache baada ya kuuawa kwao, Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Andrew Mhando Daraja, alisema polisi wa Detroit walikuwa wakiendelea na uchunguzi wa tukio hilo la kikatili lililofanywa na watu wasiojulikana na kwa sababu ambazo hadi hivi sasa hazijaweza kubainishwa.
Habari nyingine kutoka huko Detroit zilikuwa zikionyesha kwamba, polisi wa huko walikuwa wameahidi kutoa zawadi ya dola za Marekani 4,000 (sawa na sh milioni 5.12) kwa mtu yeyote atakayefanikisha kukamatwa kwa watu waliohusika katika tukio hilo baya na la aina yake kwa Watanzania wanaoishi nje ya nchi.