Halmashauri ya wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma inatarajia kuwachululia hatua za kinidhamu watumishi wake wanaoshindwa kuwahudumia watoto wao walioko katika shule za sekondari.
Kauli hiyo imetolewa na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kibondo wiki hii wakati akihutubia katika mahafali ya kidato cha nne katika shule ya sekondari Malagarasi wilayani humo.
Akihutubi kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji Bw. Naoshon Kababaye ambaye ni afisa utumishi wa halmashauri hiyo amewataka wanafunzi kutoa taarifa kwa mkurugenzi endapo wazazi wao watashindwa kuwahudumia kielimu.
Bw. Kababaye amebainisha kuwa halmashauri imekuwa ikipokea malalamiko mengi yasiyo rasimi yanayowashutumu baadhi ya watumishi wake wanaoshindwa hata kuwalipia ada watoto wao.
Amesema kitendo hiki ni cha aibu kwa mtumishi na kwamba halmashuri itaanza kuwashughulikia watumishi wenye tabia hiyo ili kuhakikisha watoto wao wanapata elimu inayostahili.
Kwa upande wake mkuu wa shule ya sekondari malagarasi Josephat Ntabindi ameahidi kutoa ushirikiano kwa halmashauri ili kuondoa kero ya ada kwa wanafunzi ambao wazazi wao ni watumishi.
Awali akitoa taarifa ya shule mkuu huyo alisema shule yake inakabiliwa na matatizo makubwa ya kukosa misaada kutoka halmashauri ya wilaya, ukosefu wa walimu, na baadhi ya wazazi wakiwemo watumishi kuwatelekeza watoto wao kwa kutolia ada kwa wakati.