OFISI ya Rais (Ikulu), imesema imeshtushwa na kushangazwa na katuni iliyochorwa katika gazeti la Kenya la Sunday Nation la Jumapili iliyopita inayomuonyesha Rais Jakaya Kikwete akilambwa viatu na waandishi wa vyombo vya habari hapa nchini.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa simu jana, Mwandishi Msaidizi wa Habari wa Rais, Maura Mwingira alisema Ikulu imeiona picha hiyo na kuichukulia kuwa ni dhihaka mbaya kwa Rais Kikwete na kwa vyombo vya habari hapa nchini.
Mwingira alisema pamoja na kulitambua hilo, Rais Kikwete ameamua kukaa kimya akiendeleza msimamo wake wa kawaida wa kutotaka kuingia katika malumbano ya aina yoyote na vyombo vya habari.
“Ni kweli tumeiona ile katuni. Ni mbaya. Rais kama ilivyo kawaida yake hangependa kuendeleza malumbano na vyombo vya habari, lakini kwa kweli sasa hawa Wakenya wamefika pabaya kwani wameamua kumdhalilisha rais wetu aliyechaguliwa kwa asilimia 80 ya kura na Watanzania.
“Sisi Watanzania kwa hulka ni waungwana na watu tusiopenda malumbano kama ilivyo kwa wenzetu hao. Wanapaswa kutambua kuwa, Kikwete ni kiongozi wa nchi anayepaswa kuheshimiwa. Hata kama kuna uhuru wa vyombo vya habari, nadhani kwa katuni ile huo si uhuru, ni dharau,” alisema Maura.
Alisema pamoja na wao (Ikulu) kukaa kimya, ana imani kwamba, vyombo vya habari hapa nchini, vina wajibu wa kutokaa kimya katika hili kwani, katuni hiyo nayo inaonyesha kwamba waandishi wa habari wanamlamba Rais Kikwete viatu, jambo alilolielezea kuwa ni udhalilishaji wa taaluma ya uandishi.
Katuni hiyo imeendelea kuthibitisha kwa namna nyingine kwamba, kumekuwa na hali ya baadhi ya wananchi na viongozi wa Kenya kutoiamini na wakati mwingine kuonyesha dharau za wazi kwa Serikali ya Rais Kikwete.
Septemba 19 mwaka huu, vyombo vya habari vya Kenya vikiongozwa na gazeti la Nation ambalo ni gazeti dada la Sunday Nation, vililivalia njuga suala la mkutano kati ya Rais George W. Bush wa Marekani na Rais Kikwete uliofanyika New York, Marekani, muda mfupi kabla ya kuanza kwa kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, ambacho Kikwete alihudhuria kwa mara ya kwanza akiwa rais.
Uamuzi wa Wakenya kuvalia njuga suala hilo ulikuja baada ya Mshauri wa Masuala ya Afrika wa Rais wa Marekani, Cindy Courville kuwaeleza waandishi wa habari kuwa, hali ya kukosekana kwa utangamano wa kisiasa nchini Kenya, lilikuwa moja ya mambo yaliyojadiliwa wakati wa mkutano wa viongozi hao wawili.
Taarifa hiyo ya Courville ilisababisha gazeti la Nation kuibua mjadala kuhusu suala hilo, hata kufika hatua ya kuandika maoni ya mhariri likihoji sababu za Bush kuijadili Kenya akiwa na Kikwete pasipo kuwashirikisha viongozi wa nchi hiyo (Kenya) waliokuwa wakiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo, Raphael Tuju aliyekuwapo huko huko New York.
Pamoja na taarifa za gazeti hilo kueleza katika sehemu fulani kwamba, Tanzania imekuwa na uhusiano mzuri na Kenya, hususan katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, maoni na habari zilizoandikwa katika gazeti hilo zilionyesha dhahiri dharau kwa Kikwete na Tanzania.
Mbali ya gazeti la Nation, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Moses Wetang’ula naye aliingia na kueleza kushangazwa kwake na uamuzi huo wa Bush kuijadili Kenya akiwa na Kikwete na pia kuzungumzia hali ya kutotengemaa, wakati akijua kuwa nchi hiyo ilikuwa na amani na utulivu.
Akizungumza kuhusu suala hilo alipokuwa akizungumza na wahariri wakuu wa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam juzi, Kikwete kwa ufupi na huku akisema ‘tusifike mbali zaidi’, alisema katika mazungumzo yao, Rais Bush alitaka tu kujua iwapo kelele za kisiasa anazosikia kutoka Kenya zitaendelea kuliacha taifa hilo katika hali ya amani.
“Nilichokiona mimi katika mazungumzo yale ni kwamba Rais Bush aliuliza kama rafiki na wala si zaidi ya hapo... tusifike mbali zaidi,” alisema Kikwete akionyesha namna ambavyo hakuwa tayari kueleza hisia zake waziwazi kuhusu suala hilo.
Kwa muda mrefu sasa na hasa tangu serikali ilipowafukuza waandishi wapatao sita wa habari wa Kenya, wote wakitokea gazeti la Nation, kwa kosa la kufanya kazi nchini kinyume cha sheria mapema mwaka jana, kumekuwa na uhusiano wa shaka kati ya nchi hizi mbili.
Miongoni mwa waandishi hao wa Kenya waliofukuzwa ni Mutuma Mathiu ambaye hivi sasa ndiye Mhariri Mtendaji wa gazeti la Sunday Nation ambalo juzi Jumapili limetumia katuni hiyo iliyobeba ujumbe wa dhihaka.
Wakati Nation wakiwatuhumu waandishi wa Tanzania kwa kuikumbatia Serikali ya Kikwete, gazeti hilo katika hali ya uwazi kabisa ndilo lililoongoza harakati za kuhakikisha Rais Mwai Kibaki na chama cha muungano wa vyama uliounda Narc wanaingia madarakani na kukibwaga chama cha Kanu ambacho ndicho kilichokuwa kikiongoza nchi hiyo tangu uhuru mwaka 1962.
Hata hivyo, tuhuma za rushwa na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora vilisababisha magazeti hayo kulazimika kubadili msimamo wake wa kuiunga mkono Serikali ya Kibaki.