WAZIRI Mkuu, Edward Lowassa kwa mara nyingine ametetea safari za Rais Jakaya Kikwete nje ya nchi na kusema anachofanya huko na hasa Marekani ni kuchangamkia fedha za Millennium Challenge Account takribani sh bilioni moja.
“Hata kama kuna watu wanaichukia Marekani, lakini ukweli unabaki pale pale kuwa Marekani ni taifa kubwa na Rais Bush tayari amekwishaonyesha nia ya kufanya kazi na Tanzania kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo,” alisema Lowassa.
Alisema kama watu walikuwa wakifuatilia kwenye vyombo vya habari, hivi karibuni Rais Bush alimwambia Rais Kikwete kuwa yeye ni rafiki yake Afrika, na ameahidi kufanya naye kazi.
“Hawa mabwana wana fedha nyingi na sisi shida yetu ni kupata fedha nyingi kutimiza ahadi yetu kwa wananchi tuliyoitoa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu, hivyo wanaosema rais anakwenda huko kupoteza muda wanakosea, anatafuta fedha," alisitiza Lowassa.
Tanzania tayari imekwishapita kwenye hatua ya kwanza ya kupata fedha kwenye mfuko huo wa Marekani na hatua ya kwanza iliyofanywa na Marekani ni kutoa fedha kwa ajili ya kupambana na rushwa.
“Halafu mtambue kuwa huko aliko rais ndiko vipo hivi vyombo vikubwa vya fedha kama Benki ya Dunia na IMF na Tanzania tayari imeonekana kuwa inaweza kufanya vizuri kwenye mabadiliko ya uchumi, lazima tuchangamke,” alisema.
Akijibu baadhi ya kero za wananchi wa manispaa, aliagiza Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Vyuo Vikuu kuhakikisha inawapa wanafunzi walioidhinishwa kupewa mikopo hiyo mara moja.
Aliwataka pia viongozi wa halmashauri hasa wanaoshughulikia suala la ardhi kumaliza migogoro iliyojikita kwenye manispaa hiyo inayohusu ardhi.