ALIYEKUWA Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, Inspekta Jenerali Omari Mahita, anatarajia kutoa utetezi wake Oktoba 17, mwaka huu katika kesi ya madai ya kumtelekeza mtoto aliyezaa na mtumishi wake wa ndani, Rehema Shaaban.
Mahita, atajitetea mbele ya Hakimu Mkazi, Pellegia Khaday wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, kutokana na maombi ya wakili, Charles Semgalawe, anayemtetea.
Wakili Semigalawe, aliiomba mahakama kuwasilisha maelezo ya utetezi wa mteja wake kwa njia ya maandishi, Oktoba 16.
Akiahirisha kesi hiyo jana, Hakimu Khaday, alikubali maombi ya wakili huyo na kusema, kesi hiyo itaendelea Octoba 17 baada ya maelezo ya utetezi kuwasilishwa mahakamani hapo.
Mdai katika kesi hiyo namba 2/2006 ni Rehema Shaabani, wakati mtoto anayedaiwa kutopewa matunzo na IGP mstaafu Mahita, ni Juma Omari Mahita.
Madai ya msingi ya mlalamikaji ni kutaka mahakama kumtambua mdaiwa kama baba halisi wa mtoto huyo na kumtaka alipe sh 100,000 kila mwezi kama matunzo ya mtoto kuanzia mwaka 1997 hadi mtoto huyo atakapomaliza shule.
Aidha, katika hati ya kiapo kilichowasilishwa mahakamani hapo na mdai, kinaeleza kwamba, uhusiano wa kimapenzi kati ya IGP huyo na ‘Housegirl’ wake ulianza Mei mwaka 1996 hadi Oktoba mwaka huo, baada ya kugundua kuwa na ujauzito wa mwajiri wake (Mahita), wakati huo alikuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro (RPC).
Sehemu ya kiapo hicho inaeleza kwamba, Mahita alimshauri Housegirl huyo kurudi kwao Kondoa ili mke wake wa ndoa (ambaye sasa ni marehemu), asifahamu kuhusu hilo na kumpa fedha taslimu sh 40,000; na kuahidi kumtunza mtoto atakayezaliwa.
Hati ya kiapo inaeleza, Mahita, alimkataza mama wa mtoto huyo, kudai matumizi ya mtoto na kumfuata kuhusu hilo. Jitihada za kutafuta suluhu ziligonga mwamba baada Mahita kudaiwa kukaidi wito wa Ofisi ya Ustawi wa Jamii, zaidi ya mara mbili.
Kesi hiyo iliyovuta hisia za watu wengi, hasa wanaharakati wa mambo ya jinsia, ilihudhuriwa na watu wengi ambao walimwona mama na mtoto huyo anayedaiwa kuwa wa Mahita.