Na Mussa Juma, Arusha
Raia saba wa Somalia wanaotuhumiwa kuingia Tanzania kinyemela wamekamatwa baada ya maofisi wa Uhamijai kuvunja chumba walimokuwa wamefichwa mjini Arusha, Kaskazini ya Tanzania.
Afisa Uhamiaji wa Mkoa wa Arusha, Justin Kabugumila jana alisema Wasomali hao waliokamatwa, wawili ni watu wazima na watoto wanaodai kuwa ni yatima baada ya wazazi wao kuuawa katika vita vinavyoendelea nchini kwao.
Wasomali hao wanadaiwa kukamatwa Jumapili iliyopita majira ya alasiri baada ya maafisa hao wa idara hiyo kwa kushirikiana na askari wa jeshi la polisi mkoani hapa.
Baada ya kuwahoji watoto hao walidai kuwa waliingia nchini kwa lengo la kwenda kumtafuta baba yao mdogo aishiye jijini Dar es Salaam baada ya kufiwa na wazazi wao.Kukamatwa kwa raia hao, kunafuatia taarifa kutoka kwa raia mwema baada ya kuwaona wakiingizwa kwenye chumba hicho na kufungiwa kwa nje.
Inadaiwa waliingizwa nchini na watoto wa mwenye nyumba hiyo.Watuhumiwa wawili ambao wenye umri juu zaidi ya miaka 18 watafikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya kuingia nchini kinyemela huku polisi ikiendelea kuwasaka watoto wa mwenye nyumba hiyo kwa tuhuma za kuwaingiza nchini Wasomali hao kinyume cha sheria.
"Hawa wengine (watoto) bado tunafanya mahojiano nao kujua ndugu zao kama kweli mmoja yupo Dar es Salaam au kama wana ndugu Nairobi Kenya ili tuwarejeshe, "alisema.