MKUU wa Jeshi la Polisi mstaafu, Inspekta Jenerali Omari Mahita (Ngunguri), leo anatarajiwa kupandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akituhumiwa kumtia mimba yaya wake, kuzaa naye na kisha kukataa kutoa fedha za matunzo.
Mahita anadaiwa kuzaa na binti huyo miaka minane iliyopita.
Kesi hiyo ya madai namba 2/2006 ilifunguliwa Agosti 10, mwaka huu mahakamani hapo na Rehema Shaabani, kwa msaada wa Kituo cha Kutetea Haki za Binadamu.
Uamuzi huo ulitokana na IGP huyo mstaafu kushindwa kumhudumia mtoto huyo kwa miaka yote, na juhudi za usuluhishi kushindikana.
Mahita katika kesi hiyo anatetewa na wakili wa kujitegemea aliyejulikana kwa jina moja la Semigalawa.
Kesi hiyo ipo mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Pellagia Khaday.
Kwa mujibu wa hati ya madai, mlalamikaji, anaiomba Mahakama imtambue Mahita kama baba halisi wa mtoto wake, na imwamuru kulipa matunzo ya sh 100,000 kila mwezi kuanzia mwaka 1997, mwaka ambao mlalamikaji alijifungua.
Hati hiyo ya kiapo inaeleza kwamba uhusiano wa kimapenzi kati ya Mahita na yaya wake ulianza Mei 1996 hadi Oktoba 1996, wakati huo Mahita akiwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa (RPC) wa Kilimanjaro.
Mlalamikaji anadai kuwa, wakiwa katika uhusiano huo wa kimapenzi, alipata ujauzito. Mdaiwa alimpa sh 40,000 na kumshauri arudi kwao Kondoa, ili mke wa ndoa wa Mahita (ambaye sasa ni marehemu), asifahamu kilichokuwa kikiendelea.
Mlalamikaji anasema kuwa makubaliano hayo yalifikiwa kwa masharti ya kumtaka Mahita amhuhudumie mtoto atakayezaliwa.
Mtoto alizaliwa mwaka 1997 na kupewa jina la Juma, baba wa mtoto (Mahita), na aliahidi kutoa matunzo.
Inadaiwa kwamba hakuna siku ambayo Mahita aliwahi kumkana mtoto huyo.
“Alinikataza kumfuata ofisini na nyumbani kumdai matunzo ya mtoto,” inaeleza sehemu ya hati ya kiapo cha yaya huyo.
Anadai kuwa juhudi za mdai huyo za kutaka usuluhishi wa suala hilo ziligonga mwamba baada ya Mahita, kukaidi amri za kuitwa kwenye ofisi za ustawi wa jamii na mabaraza mbalimbali tangu mwaka 2003.
Hali hiyo ilisababisha mlalamikaji kufikia uamuzi wa kutafuta msaada wa kisheria na kufungua kesi.
Hati hiyo ya kiapo ilieleza kwamba, Mahita, alimtuma askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia, aliyejulikana kwa jina la Peter, na mfanyakazi wake mvulana aliyetajwa kwa jina la Hussein, ambao walimchukua mtoto na kumpeleka kusikojulikana.
Mdai aliamua kufuatilia aliko mtoto huyo, na alikamatwa na kupelekwa Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam, na kubambikiwa makosa asiyoyafahamu.
Baada ya kukaa rumande kwa siku kadhaa, watu anaoamini kuwa walitumwa na Mahita, walimchukua na kumpeleka katika nyumba iliyopo Mkwajuni kwa Sheikh Yahaya, na kufanikiwa kumwona mtoto wake.
Mdai anasema tangu wakati huo, hajamwona tena mtoto huyo, na kwa sababu hiyo, anataka arudishiwe mwanawe, na alipwe kiasi cha fedha alichokitumia kwa matunzo kwa muda wote aliokuwa naye.
Kesi hiyo inatarajiwa kuvuta hisia za wengi, hasa wanaharakati wa haki za wanawake na watoto.