SERIKALI imesema makali ya mgawo wa umeme yatapungua wiki ijayo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, mara baada ya kutembelea mitambo ya gridi ya taifa na Songas, Ubungo, Dar es Salaam, jana, Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Ibrahim Msabaha, alisema hali hiyo imetokana na juhudi kubwa zinazofanywa na kampuni zilizopata zabuni ya kufunga jenereta na kuanza kutumika kwa gesi ya Songo Songo.
“Nawahakikishia Watanzania kuwa, kuanzia mwishoni mwa wiki ya kwanza ya mwezi Oktoba, hali ya mgawo huu itapungua zaidi kwa vile megawati zitakazozalishwa zitakuwa zimeanza kukidhi mahitaji ya kila siku,” alisema Dk. Msabaha.
Alisema hadi jana jioni mtambo wa kuzalisha megawati 40 ulikuwa umefungwa chini ya Kampuni ya Songas; na megawati 35 zitapatikana kuanzia leo jioni.
Alisema kutokana na mafanikio hayo, safari ya kuondokana na tatizo hilo imeanza kuonekana.
“Baada ya kutembelea maeneo yote kunakofungwa jenereta, nimeridhika na shughuli zinavyokwenda, hivyo basi tumuombe Mungu ili neema hii iweze kuja haraka,” alisema Dk. Msabaha.
Alisema kulingana na mafanikio hayo, ratiba ya mgawo wa umeme itabadilika kuanzia leo. Umeme utakatwa kuanzia saa 12 asubuhi na kurudishwa saa 11, jioni baadala ya saa moja.
“Ratiba hii imebadilika kidogo baada ya kukutana na viongozi wa madhehebu ya dini ambao walitueleza masuala mbalimbali na hivyo tukaona ni vyema kuanzia sasa umeme urejeshwe kuanzia saa 11 jioni,” alisema Dk. Msabaha.
Alisema pia serikali inafanya mpango wa haraka wa kuwatoa kwenye mgawo huo wamiliki wa viwanda ili kuepusha matatizo na kushuka kiwango cha uzalishaji.
Alisema hadi jana jioni, meli yenye jenereta 12 ilitarajiwa kutia nanga katika Bandari ya Dar es Salaam ikitokea Houston, Marekani. Upakuaji ulitarajiwa kuanza leo na zitafikishwa Ubungo kabla ya Jumamosi wiki hii.
“Mbali ya jenereta hizi, pia Kampuni ya East Energ (ECE/PAE) imekwishafanya maandalizi yote kwa ajili ya ufungaji wa mabomba ya gesi asilia ili ikifikishwa ifungwe na gesi iweze kuunganishwa,” alisema Dk. Msabaha.
Kuhusu mtambo wa kukodisha kutoka Kampuni ya Richmond Development ya Marekani, ambao unazalisha megawati 100, alisema unatarajiwa kuwasili nchini Oktoba 8, mwaka huu