Na Mwandishi wa HabariTanzania.com Arusha.
HUENDA tatizo la uharibifu wa mazingira kwenye maeneo ya migodi likaisha baada ya moja ya kampuni kutoka nchini Uingereza kugundua chombo maalum kijulikanacho kama (Short Range Mineral Detector)kwaajili ya kugundua eneo halisi ambalo madini yamekuwa yakipatikana juu ya ardhi na ndani ya migodi.
Akizungumza na majira jana mjini hapa Mkurugenzi wa kampuni ya Robinson and Company Ltd ya nchini Uingereza Bw. Mathew Robinson alisema chombo hicho kinachotumia mionzi maalum kimekuwa kikigundua eneo halisi yalipo madini.
Alisema baada ya utafiti wa muda mrefu kuhusiana na chombo hicho kwa kushirikiana na wamiliki mbalimbali wa machimbo ya madini katika nchi za Afrika Mashariki kampuni hiyo imepanga kuanza rasmi kazi ya kugundua maeneo yalipo madini katika nchi hizo kazi ambayo inatarajiwa kuanza Oktoba mwaka huu.
Hata hivyo Bw.Robinson alisema hivi sasa wamiliki wa migodi watapewa huduma hiyo bure bila ya kuchajiwa kiasi chochote cha fedha na kwamba kampuni hiyo imeshaweza kugundua maeneo mengi yenye madini nchini ikiwemo mkoani Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Morogoro,Rukwa na Singida.
Bw.Robinson alisema chombo hicho kimekuwa kikigundua madini aina ya Tanzanite ambayo yamekuwa yakipatikana katika migodi ya Mirerani wilayani Simanjiro Pekee na Green Gamet na Red Gamet, Spinel( ulanga) ambayo yamekuwa yakipatikana maeneo mengi nchini.
"kwa kutumia chombo maalum tumeweza kugundua maeneo mengi ya awali yenye madini, hata hivyo kwa sasa chombo ambacho tunacho kimekuwa kikiona madini yaliyopo umbali wa mita 300 hadi 500 upana na mita 30 kwenda ardhini kutegemeana na aina ya mwamba ambao madini hayo yamekuwa yakipatikana...chombo hiki ni tofauti ya vyombo ambavyo vimekuwa vikitumika kutafuta madini ya aina ya dhahabu ambayo ni ya chuma,SRMD ni maalum kwaajili ya madini kama ya Tanzanite ambayo yanatokana na chupa na mengineyo ya aina hiyo ,"alisema.
Alisema kampuni ya Robinson iliamua kufanya utafiti wa chombo cha kugundua eneo ambalo madini aina ya Tanzanite ambapo yamekuwa yakipatikana kwa kuwa tangu madini hayo kugunduliwa duniani hakuna chombo kilichowahi kutegenezwa kwa ajili ya kugundua uwepo wa madini hayo.
Akitolea mfano wachimbaji wa madini ya Tanzanite yanayopatikana nchini pekee, Bw.Robinson alisema watu wamekuwa wakitumia muda wao mwingi pamoja na fedha nyingi kuchimba madini hayo kwa kuwa wamekuwa wakikosa chombo kinachoonyesha eneo halisi ambalo madini hayo yamekuwa yakipitikana.
" Kwa kutumia chombo hiki wamiliki wa migodi wa Afrika Mashariki wataweza kuondokana na adha ya kutafuta madini hayo sanjari na kuokoa fedha ambazo wamekuwa wakizitumia bila ya kuwa na vipimo, kwa sasa tunatoa huduma hii bure na kwa wale wanaotaka wawasiliane na sisi kwa kutembelea mtandao wa
www.habaritanzania.com watatusoma,"alisema Bw.Robinson.
Alisema pia wamiliki wa machimbo hayo wataweza kugundua maeneo mengine yenye madini na kuendeleza shughuli hiyo kwa muda mrefu zaidi tofauti na sasa ambapo wamekuwa wakikata tamaa kufuatia kutafuta madini hayo kwa muda mrefu bila ya mafanikio.
kuhusu uharibifu wa mazingira katika maeneo ya migodi Bw.Robinson alisema kwa kutumia chombo hicho wachimbaji watakuwa hawachimbi ovyo kila eneo kwaajili ya kutafuta madini na badala yake watakuwa wakichimba eneo halisi lenye madini.
Contacts:
Robinson & Company International Ltd
Mobile: +255 78 498 9868
Email: info@habaritanzania.com