GENGE la wahalifu limeibuka jijini Dar es Salaam, likijihusisha na utengenezaji wa noti bandia, Tanzania Daima imebaini.
Wahusika wa uhalifu huo wapo Mtaa wa Mkadini, Magomeni, jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya watu wameiambia Tanzania Daima kuwa wahalifu hao wana mtambo wa kutengeneza fedha za Tanzania na Kenya.
Suala hilo limeshafikishwa katika vyombo vya dola, lakini hakuna dalili za kulishughulikia kwa lengo la kulitokomeza.
Baadhi ya viongozi eneo la Magomeni walioomba majina yao yahifadhiwe, wamethibitisha kuwapo kwa uhalifu huo, na kushangaa kasi ya polisi ya kulimaliza tatizo hilo.
Walisema pamoja na utengenezaji wa noti bandia, pia kumeshamiri biashara ya mihadarati.
Baadhi ya watuhumiwa, wameamriwa kulihama eneo hilo.
Mmoja wa waliokuwa wadaiwa wa biashara hiyo, alisema noti ya sh 10,000 hununuliwa na walanguzi kwa sh 3,000.
Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ilishakataa kata kata kuwa noti za sasa haziwezi kughushiwa kirahisi.
Hata hivyo, Jeshi la Polisi, kupitia kwa aliyekuwa msemaji wake, Aden Mwamunyange, lilisisitiza kuwa noti bandia zipo mitaani, na kwamba ushahidi upo.