MMOJA wa washiriki wa filamu inayoonyesha utumikishaji watoto katika machimbo ya tanzanite, Mererani, Harry Mushi, amemtetea Mbunge wa Viti Maalumu, Dorah Mushi, akisema hakushiriki kuandaa filamu hiyo.
Taarifa ya Harry kwa Tanzania Daima, aliyotoa jana, ilisema filamu hiyo ilifadhiliwa na Umoja wa Mataifa na kutayarishwa na IRIN TV.
Alisema baraka zote za upigaji picha, zilitolewa na serikali chini ya Idara ya Habari (MAELEZO).
“Wakati filamu inatayarishwa, watoto zaidi ya 3,000 walishaondolewa katika uchimbaji huo na tafiti zilionyesha kuwapo kwa watoto zaidi ya 4,000,” alisema Harry.
Akimtetea mbunge huyo, alisema: “Wakati picha zinachukuliwa, Mheshimiwa alishakuwa mbunge tayari. Aliteuliwa Septemba, 2005 na picha zilichukuliwa Novemba 2005, kwa hivyo inapoelezwa kuwa mbunge alihusika kwa hali na mali, si kweli na wala hakuhojiwa na IRIN TV jambo lolote.”
Hata hivyo, mbunge huyo ni mmoja wa waasisi na viongozi wa shirika lisilo la kiserikali la Good Hope lenye makao yake Mererani, Manyara.
Ufafanuzi wa Harry umekuja baada ya kuwapo habari kwamba mbunge huyo alianza kushiriki uandaaji wa filamu hiyo kutokana na dhima ya shirika lake.
Dhima kuu ya shirika hilo ni kupambana na hatimaye kutokomeza ajira mbaya ya watoto, likianzia na watoto waliopo machimboni Marerani