Hivi karibuni mameya wa majiji ya Madrid nchini Hispania na Milano nchini Italia wamepania kuangalia upya suala zima la ushiriki na viwango katika mashindano ya mitindo na mavazi kwenye majiji yao.
Kwa taarifa zilizovifikia vyombo vya habari ni kwamba kuanzia sasa kutakuwa na viwango maalumu kuhusu umbo na uzito wa washiriki kulingana na takwimu kutoka nchi husika.
Hii imefikiwa baada ya kufahamika kuwa wasichana wengi wanaoshiriki urembo au maonyesho ya mavazi wanaishi maisha ya mateso ya kujikondesha ili kukidhi viwango vinavyotakiwa na waandaji wa mashindano hayo.
Katika dhana iliyojulikana kama wearing thin, wanaopinga ukimbau mbau huu wamesema kuwa wahusika wanateseka bila sababu na hili ni uvunjaji wa haki za binadamu.
Dina Memerenko toka Urusi alikiri kuwa hata wahusika wanahisi hivyo ila kwa vile hawana la kufanya bali wanahitaji pesa, hujikuta wakikabiliana na hayo mateso ili wapate pesa.
Alitoa mfano wa rafiki yake ambaye hakumtaja jina kuwa alikuwa akiishi kwa kula apple moja kila siku kwa siku tatu kabla ya kupanda jukwaani.
Meya wa Milano ambao husifika kama mji mkuu wa urembo na mitindo amebainisha wazi kuwa mifupa au ukondefu au ukimbau mbau huumiza mwili na akili. Hivyo ni mateso sawa na mateso mengine lazima yapigwe vita na kukomeshwa.
Kwa wafuatiliaji wasiopenda mifupa inayoonyeshwa mara nyingi kwenye majukwaa ya huko nyumbani, watapata lau pumzi maana hadi hili linatokea,nchi hasa za kiafrika zilikuwa zinafuata mkumbo tu bila kujali haiba inayovutia ya jamii ya kiafrika.
Kwa kuliona hili tunaamini binti zetu watapata nao ahueni kutokana na mateso na utumwa wa urembo na mitindo.