VIONGOZI wametakiwa kuwaelimisha wananchi umuhimu wa kuchangia ujenzi wa shule.
Wito huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na wanaharakati wa kwenye semina za maendeleo za kila wiki (GDSS), zinazoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP).
Wanaharakati hao walisema uelewa mdogo kwa wananchi kuhusu kuchangia ujengaji wa shule ni kikwazo kikubwa kinachowafanya washindwe kuchangia.
“Mfano utamkuta mtu anasema: ‘Hiyo shule hata nikitoa mchango ni nani atakayesoma, watoto wangu wote wamekwisha kuolewa, lakini asijue kuwa kuna mjukuu wake ambaye anaweza kusoma baadaye kwenye shule hiyo,” walisema wanaharakati hao.
Mtoa mada ambaye ni Mwenyekiti wa Mfuko wa Elimu wa Wilaya ya Kinondoni, Teopilas Kahingwa, alisema kutokana na upungufu wa shule katika wilaya hiyo wanafunzi wengi wameshindwa kujiunga na shule za sekondari na hivyo kujiingiza kwenye vitendo viovu.
Mmoja wa wachangiaji kwenye semina hiyo, Msafiri Shabani, alipendekeza shule zijengwe nje ya mji na si katikati ambako kuna msongamano mkubwa.
Alisema shule zikijengwa nje ya mji zitahamasisha serikali kupeleka huduma nyingine za msingi zikiwamo maji, umeme, barabara na hospitali.