WAATHIRIKA wa ugonjwa wa UKIMWI mkoani Rukwa, wametakiwa kufanya shughuli zao kwa kushirikisha vyombo vya habari ili waweze kusonga mbele kimaendeleo.
Hayo yamesemwa jana na Mwenyekiti wa Chama cha Waathirika wa UKIMWI (SHIDEPHA+), mkoani Rukwa, Godfrey Mwikala katika uchaguzi wa chama hicho ngazi ya wilaya iliyohusisha Halmashauri ya Manispaa ya Wilaya ya Sumbawanga.
Mwikala alisema: “Waathirika wenzangu najivua leo madaraka ya uwenyekiti kwa chama hiki, lakini napenda kuwaambia kuwa tumieni vyombo vya habari kwa kila mtakachokifanya, msiwaogope waandishi, hawa ni chombo muhimu sana katika shughuli zenu.”
Alisema SHIDEPHA+ mkoani Rukwa, bila vyombo vya habari isingejulikana mahala popote pale, lakini kwa sasa chama hicho kinajulikana nchi nzima kupitia vyombo vya habari.
Katika uchaguzi huo wa SHIDEPHA+ ngazi ya wilaya uliosimamiwa na Ozem Chapita, Salum Korongo alichaguliwa kuwa mwenyekiti kwa kupata kura zote 25 baada ya wagombea wawili kujitoa. Waliojitoa ni Winnie Kayanza na Rose Ngao