WIZARA ya Maliasili na Utalii, kwa kuwatumia wataalamu wake na wa intaneti, imefanikiwa kuingiza taarifa kwenye mtandao zikilenga kuikosoa filamu ya Darwin’s Nightmare.
Habari kutoka wizarani hapo zimesema kwamba, kutokana na ‘utundu’ huo, sasa kila anayefungua website yenye kuelezea filamu hiyo, lazima akutane na tamko la serikali kuhusu kile kinachoitwa upotoshaji uliofanywa na Hubert Sauper.
“Ukifungua google, yahoo, msn ukitafuta Darwin’s Nightmare, lazima pembeni utaona msimamo wa serikali unaotoa upande wa pili na ukweli kuhusu kile kilichopotoshwa kwenye filamu hiyo, na pia katika partner site million 21” alisema mmoja wa walioshiriki kufanikisha kazi hiyo.
Mtaalamu huyo alisema walipata msukumo wa kutekeleza wazo hilo, baada ya kushauriwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Anthony Diallo, ambaye pia ni mtaalamu wa biashara za elektroniki zinazohusu intaneti.
“Tunatarajia kuwa wasomaji milioni 50 watakuwa wamesoma taarifa halisi ya serikali katika kipindi cha miezi miwili hadi mitatu.
“Hii ni web attack, ni vita ya elektroniki, lazima na sisi tuipigane ki-eletroniki ili tupate ushindi.
“Tukipigana kwa kukanusha tu kwenye vyombo vingine vya habari, tunaweza tusifanikiwe sana kama tukitumia njia hii tuliyoamua kuitumia.
“Sasa kila atakayetaka kuijua Darwin’s Nightmare, basi hapo hapo atapata upande wa pili, yaani tamko la serikali yetu, kwa hiyo msomaji atajua kuwa filamu hii iliandaliwa kutuchafua Watanzania na kuharibu kabisa biashara ya samaki wetu Ulaya,” alisema mtaalamu huyo.
Filamu hiyo iliandaliwa mwaka 2004. Inaonyesha biashara ya samaki Ulaya na ulaji mabaki ya sangara (mapanki) kwa wakazi wa Kanda ya Ziwa.
Pia inazungumzia ukahaba na kuenea kwa UKIMWI; na usafirishaji silaha katika eneo la maziwa makuu.
Yote hayo yamekanushwa vikali na Rais Jakaya Kikwete. Lakini walioiona, wanakubaliana na mengi, isipokuwa usafirishaji silaha.
http://www.darwinsnightmare.net
Source: Tanzania Daima