Bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari Mkalamo, iliyopo wilayani Korogwe, limeteketea tena kwa moto pamoja na mali zote za wanafunzi zilizokuwemo.
Mali za wanafunzi zilizoteketea, zinakadiriwa kufikia Sh. milioni 1.5.
Hili ni tukio la pili kwa majengo ya shule hiyo kuwaka moto katika kipindi kisichozidi mwezi mmoja.
Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Bi. Betty Mkwassa, amemuagiza mkuu wa shule hiyo, Bw. Reward Kimbute kuyafunga mara moja mabweni ya shule hiyo ili kuepusha hatari zaidi inayoweza kutokea.
Bi. Mkwasa aliyefika shuleni hapo jana alisema, kitendo cha mabweni ya shule hiyo kuendelea kuungua, kinahatarisha usalama, maisha na mali za wanafunzi.
Aliagiza uchunguzi wa kina ufanyike kabla ya kuanza kutumika tena.
Aidha, Bi. Mkwasa aliwataka wakazi wa kijiji cha Kwalukonge, mahali ilipo shule hiyo, kusaidiana na uongozi wa shule katika kubaini sababu za kutokea mfululizo kwa matukio ya moto katika mabweni ya shule hiyo.
Naye Bw. Kimbute alisema moto huo ulitokea wakati wanafunzi hao wakiwa madarasani.
Bw. Kimbute alivitaja vitu vilivyoteketea kwa moto huo kuwa ni nguo, vitanda viwili mashuka, madaftari na vitu vingine vidogo vidogo mali ya wanafunzi hao.
Baadhi ya wanakijiji ilipo shule hiyo, wamehusisha matukio ya moto na imani za kishirikina.
Walidai kuwa, moto huo umesababishwa na mizimu iliyopo katika moja ya mlima uliopo jirani na shule hiyo.
Waliushauri uongozi wa kijiji cha Kwalukonge kifanye matambiko ili matukio hayo yaishe.