WAZIRI wa Habari, Utamaduni na Michezo, Muhammed Seif Khatib ameitaka Bodi mpya ya Wakurugenzi ya kampuni ya magazeti ya serikali (TSN) kwamba wanawajibu wa kueleza utekelezaji wa Ilani ya CCM.
Khatib alisema hayo jana alipokuwa akizundua Bodi hiyo kwenye Hoteli ya New Africa. Wajumbe wa Bodi hiyo ni Mwenyekiti Ador Mapunda, Katibu wa Bodi Issac Mruma ambaye ni Mhariri Mtendaji mpya wa TSN inayochapisha magazeti ya Daily News na Sunday News.
Wajumbe wengine ni Balozi Peter Kallaghe, Profesa Amandina Lihamba na Habbi Gunze. Alisema serikali iliyopo madarakani ni ya CCM na gazeti hilo linapaswa kuandika utekelezaji wa Ilani ya CCM bila aibu.
Khatib alisema pia moja ya majukumu ya bodi hiyo ni kuhakikisha TSN inapata mtambo wake wa kuchapa magazeti mwaka huu kama ilivyopangwa. "Wizara yangu itajitahidi kutoa kila msaada utakaowezekana kwa niaba ya serikali kufanikisha lengo hilo," alisema.
Alisema jukumu lingine kubwa la Bodi hiyo ni kuhakikisha kuwa TSN inaanzisha gazeti la Kiswahili mapema iwezekanavyo na kwa vyovyote vile kabla ya mwisho wa mwaka huu. "Hili halina mjadala lazima lianze. Ni moja ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi," alisema.
Khatib akizungumzia chokochoko ndani ya kampuni hiyo alisema zinatokana na wafanyakazi wachache na kwa taarifa alizopata baadhi yao ni wale walioacha kazi au kupunguzwa kazi.
Alisema umefika wakati suala hili likome. Hata hivyo alishauri uongozi na menejimenti usijitenge sana na wafanyakazi na kwamba wawe karibu nao ili kuleta maelewano.
Khatib alisema wizara yake inaunga mkono uhuru wa wafanyakazi kudai haki zao za kisheria ila zifuate taratibu za kuwepo majadiliano.
"Nataka Bodi iweke mikakati ya uongozi wa kampuni na kuhakikisha nidhamu ya kazi inafuatwa na kwamba wafanyakazi pia walipwe kulingana na mchango wao kwa kampuni.
"Hii haina maana kuwa wafanyakazi wafungwe midomo ili wasilalamike hata pale wanapoonewa. La hasha. Kinachotakiwa ni kwamba taratibu za mawasiliano ya kiofisi zifuatwe bayana na madai ya haki yatolewe wazi wazi ndani ya kampuni kabla ya kupelekwa nje," alisema.
Alisema uongozi wa kampuni hauna budi kujenga mazingira mazuri ya mawasiliano na wafanyakazi watumie mfumo huo kutoa dukuduku zao.
Khatib alisema kuwa aliitaka TSN kuandika habari ziwe nzito na ukweli, zifanyiwe utafiti makini na wa kutosha na kwamba gazeti halivutii kwa habari nzito pekee yake bali upangaji wa habari na unadhifu wa gazeti nao ni muhimu.
Alisema inawabidi wawe wabunifu zaidi katika zama hizi za ushindani ili kuvutia watangazaji wa kuinua kiwango cha uchapaji na kuongeza mbinu za uuzaji ikiwemo kuboresha huduma kwa wateja.
Kutoka gazeti la Uhuru
ISSN 0876-3896 NA.19318
Na Mwandishi Wetu